Manispaa ya Sumbawanga yaibuka mshindi wa kitaifa mbio za mwenge wa uhuru

Halmashauri ya Manispaa ya Sumbawanga mkoani Rukwa imeibuka mshindi wa kitaifa wa mbio za za Mwenge wa Uhuru uliowashwa mwezi April katika viwanja vya magogo Mkoani Geita na na kuzimwa mwezi oktoba siku ya kumbukumbu ya kifo cha Mwl. Julius Nyerere katika Kiwanja Mkwakwani Mkoani Tanga na kukimbizwa katika Halmashauri 195 nchini.
Mkimbiza Mwenge wa Uhuru kitaifa Charles Kabeho ( Wa kwanza Kushoto) akifuatiwa na Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Mh. Joachim Wangabo (katikati) pamoja na Mkuu wa Wilaya ya Sumbawanga Dkt. Khalfan Haule wakati wakisubiri mwenge ukitokea Mkoa wa Katavi 

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Ajira, Kazi, Vijana na Walemavu Jenista Mhagama amesema kwamba halmashauri hiyo itapewa zawadi ya kikombe na shilingi milioni tano.
“Mheshimiwa Rais wa Zanzibar naomba sasa nimtaje mshindi wa kitaifa ambae ni Halmashauri ya Manispaa ya Sumbawanga kutoka mkoa wa Rukwa, mshindi huyu watapewa zawadi ya kikombe cheti na fedha taslimu shilingi milioni tano,” Mhagama alisema.

Manispaa ya Sumbawanga ilitumia zaidi ya Shilingi Bilioni 11.2 katika miradi 10 ikiwemo, ujenzi wa kituo cha afya Mazwi, ujenzi wa Zahanati katumba azimio, miradi minne ya maji, ujenzi wa shule mpya, ujenzi wa barabara zaidi ya Km 5.
Wengine ambao wamechukua ushindi na kupewa kikombe na cheti ni Mkoa wa Geita kwa Kuwasha mwenge huo, Mkoa wa Tanga kwa kuuzima mwenge huo, na washindi wengine wa kanda tano ambao watapewa cheti, kikombe na fedha taslim shilingi milioni moja ni Halmashauri ya Jiji la Arusha, Halmashauri ya Wilaya ya Kishapu, Halmashauri ya Wilaya ya Mbulu, Halmashauri ya Wilaya ya Chalinze na Wilaya ya kusini.

Comments