Waalimu wa Sekondari ya Itwelele wapongeza ujenzi wa maabara ya Fizikia


Walimimu pamoja na wanafunzi wa shule ya sekondari Itwelele wameipongeza Ofisi ya Mkurugenzi wa Manispaa ya Sumbanga kwa kuweza kukamilisha ujenzi wa maabara ya Fizikia iliyokuwa hitajio kubwa la shule hiyo ili kutoa wataalamu wa somo hilo.

Maabara ya Shule ya Sekondari Itwelele

Maabara hiyo iliyokamilika mwanzoni mwa mwezi wa tano mwaka huu imegharimu shilingi milioni 45, huku serikali kuu ikichangia shilingi milioni 30, wananchi nao wakichangia shilingi milioni 10 na Manispaa kuchangia shilingi milioni 5.


Mmoja wa waalimu wa sayansi katika shule hiyo James Mwambije amesema kuwa ameona nia ya serikali katika kuhakikisha inatekeleza sera ya Tanzania ya viwanda kwa kuweka mazingira mazuri ya kujifunzia kwa wanafunzi ili kuzalisha wataalamu wa kutosha.

“Dunia tuliyonayo sasa ya Sayansi na Teknolojia inawahitaji sana wataalamu watakaoweza ‘ku-operate’ (kuendesha) mitambo katika viwanda mbalimbali ambavyo ndio nia ya serikali yetu, sasa haya mazingira wanayotuwekea ndio hasa yatakayowezesha Tanzania kufikia ndoto yake,” Alisema.

Kwa upande wake Hamisi Ulaya akiongea kwa niaba ya wanafunzi wenzake amesifu juhudi za serikali za kuboresha huduma za elimu bila ya upendeleo na kuongeza kuwa ifike wakati watu wasione tofauti ya kusoma Dar es salaam na Sumbawanga.

Halmashauri ya manispaa ya Sumbawanga imetenga kiasi cha shilingi 234,656,000/= katika bajeti ya mwaka wa fedha 2017/18 kwa ajili ya ukamilishaji wa vyumba vya maabara katika shule za Sekondari 17.

Comments