"Jumla ya Vijiji 53 kupatiwa huduma ya maji" - Kasim Majaliwa



WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amesema jumla ya vijiji 53 vya mkoa wa Njombe vitapatiwa huduma ya maji safi na salama katika mwaka huu wa fedha.

Alitoa kauli hiyo jana (Jumamosi, Januari 21, 2017) wakati akizungumza na wananchi wa wilaya ya Wanging’ombe katika mkutano wa hadhara katika kata ya Ilembula.

Waziri Mkuu alisema zaidi ya sh. bilioni 2.4 zimetengwa kwa ajili ya kugharamia mradi huo wa maji katika miji ya Makambako, Njombe na wilaya ya Wanging’ombe.

Alisema kati ya vijiji hivyo vitakavyopatiwa maji, vijiji 22 ni vya wilaya ya Wanging’ombe, hivyo aliwaomba wananchi hao kuwa na subira.

Kwa mujibu wa Waziri Mkuu tayari zabuni ya mradi huo imeshatangazwa, hivyo amewaagiza viongozi wa Wizara ya Maji na Umwagiliaji watafute mkandarasi mzuri.

Alisema lengo la Serikali ya Awamu ya Tano ni kuhakikisha kila mwananchi anapata huduma ya maji katika umbali usiozidi mita 400 kutoka mahali anapoishi.

Waziri Mkuu alitoa kauli hiyo baada ya Mbunge wa Wanging’ombe, Mheshimiwa Mhandisi Gerson Lwenge kumuomba awasaidie katika kutatua kero ya maji.

Mbunge huyo ambaye pia ni Waziri wa Maji na Umwagiliaji alisema “Mheshimiwa Waziri Mkuu sisi tunakabiliwa na changamoto ya maji, leo tunaomba ututatulie kero hii”.

Changamoto nyingine aliyoitaja Mheshimiwa Lwenge ni pamoja na ukosefu wa hospitali ya wilaya, ambapo Waziri Mkuu aliigiza halmashauri hiyo kuanza ujenzi.

Alisema Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2015/2020 inaelekeza kuwa na hospitali katika kila wilaya, kituo cha afya kwa kila kata na zahanati kwa kila kijiji.

Katika hatua nyingine Waziri Mkuu alimuagiza Mkuu wa Wilaya hiyo Bw. Ally Kasinge kukutana na viongozi wa kata na vijiji vinavyozunguka hifadhi ya Mapanga Kipengele ili kutatua kero ya mpaka.
                   
(Mwisho)


Comments