Vijiji 17 vya Manispaa ya Sumbawanga kufaidika na miradi ya maji.



Halmashauri ya Manispaa ya Sumbawanga ipo mbioni kukamilisha miradi ya maji inayofadhiliwa na benki ya Dunia kwa kushirikiana na serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia programu ya maji na usafi wa mazingira vijijini (NRWSSP) ili kukata kiu ya wananchi katika kupambana na shida ya maji. 

Haya ni kutokana na azma ya serikali ya kuongeza upatikanaji wa huduma ya maji safi na salama kufikia asilimia 72 vijijini na asilimia 95 mijini hadi ifikapo mwaka 2025. 


Mwananchi akichota maji kijiji cha Malonje - Sumbawanga

 “Kwa sasa katika Manispaa ya Sumbawanga, vijijini vilivyofikiwa na huduma ya maji ni asilimia 49.9 na mjini ni asilimia 62.” Mhandisi wa maji wa Manispaa Bi. Kazoya alisema.  

Miradi hiyo inalenga kuhusisha vijiji vya Mlanda, Pito, Malagano, Tamasenga, Malonje, Kisumba, Matanga, Kasense, Chipu, Mponda, Mawenzusi, Katumba Azimio, Nambogo, Chelenganya, Luwa, Kanondo na Milanzi.

Miradi mitano inayohusisha vijiji vya Kanondo, Mlanda, Pito, Malagano, Tamasenga na Malonje inaelekea kukamilika na inatarajiwa kuhudumia wananchi 40,492 kwa miaka kumi ijayo.


Akitoa mfano wa mradi unaotarajia kuisha, Afisa wa maji wa Manispaa ndugu John Mlwafu alisema “mradi huu wa Pito, Malagano na Tamasenga unajegwa na Mkandarasi Girison Investment Co. Ltd kwa gharama ya shilingi Milioni 532 bila VAT, na mpaka sasa mradi huu umefikia asilimia 80 ya matengenezo.”

Afisa wa Maji, John Mlwafu akifafanua Mradi kwa wafanyanyazi wenzake.
Mlwafu aliongeza kuwa mradi huo ulitakiwa kuisha tangu Februari 02 mwaka huu, lakini kutokana na changamoto zilizo nje ya uwezo jambo hilo halikuweza kukamilika. 

“Mvua nyingi zilizonyesha ziliathiri kwa kiwango kikubwa sana kasi ya ujenzi wa miradi, lakini pia wakandarasi kuwa na miradi mingi kuliko uwezo wao,” Mlwafu alisisitiza.

Tanki la Maji Malonje
Katika kujiletea maendeleo vijijini na mijini, jamii inapaswa kuchangia asilimia 2.5 ya gharama za miradi ili nao waweze kuilinda na kuitunza na kuifanya ni ya kwao kwa faida yao.

Comments